Changamoto za Uchanganuzina Ufasiriwa Ushairi Katika Shule za Upili Nchini Kenya

Kariuki, Gakuo Joseph (2014) Changamoto za Uchanganuzina Ufasiriwa Ushairi Katika Shule za Upili Nchini Kenya. Masters thesis, Kenyatta University.

[img] PDF (Changamoto za Uchanganuzina Ufasiriwa Ushairi Katika Shule za Upili Nchini Kenya)
Gakuo Joseph Kariuki.pdf - Accepted Version
Restricted to Repository staff only

Download (121MB) | Request a copy

Abstract

Utafiti huu umechanganua suala la ufasiri na uelewekaji wa ushairi wa Kiswahili miongoni mwa wanafunzi wa shule za sekondari, Kenya. Ushairi ni somo la lazima shuleni na ambalo kwa muda mrefu sasa limewakanganya wanafunzi wa sekondari. Ripoti za baraza la mitihani la kitaifa zimedhihirisha matokeo mabaya ya mtihani wa Kiswahili hususan kutokana na somo la ushairi. Hali hii imewavutia wachunguzi na watafiti wengi kujaribu kuchangia suluhisho la kudumu kwa tatizo hili. Utanzu wa ushairi ndio mkongwe zaidi na wenye utata na mgogoro tangu jadi. Madhali hata tamthilia au riwaya ngumu huitwa ya kishairi. Uchunguzi huu ulijikita katika mtazamo wa nadharia za Ki-Hemenitiki na Uhistoria mpya. Utafiti ulinuia kutathmini jinsi ukengeushi wa Ki-Hemenitiki na kitamaduni unavyochangia ugumu wa ufasiri na uelewekaj i wa ushairi wa Kiswahili.Ili kuafikia lengo hili la udadisi, utafiti ulihusisha tungo mbalimbali za ushairi kutoka kwa Sauti ya Dhiki (Abdilatif Abdalla), Pambo la Lugha (Shaaban Robert), Kina cha Maisha (Said A. Mohamed). Utafiti huu ulijikita maktabani na nyanjani. Maktabani, utafiti ulinufaika na udurusu wa vitabu, miswada, majarida, tasnifu, makala na machapisho yaliyoangazia masuala ya nadharia, ushairi, uchanganuzi na tafiti kuhusu ugumu wa ufasiri wa mashairi kwajumla. Nyanjani, utafiti ulijikita katika kaunti ya Trans Nzoia na ya Mombasa. Tulitumia sampuli ya Kimakusudi iliyohusisha wanafunzi wa kidato cha tatu na cha nne. Jumla ya wanafunzi kumi waliteuliwa kutoka katika shule nne za kila kaunti. Shule hizo zilikuwa za kategoria tatu: Kitaifa, Kimkoa na Kiwilaya. Suala la kijinsia lilizingatiwa huku uteuzi wa sampuli ukiegemezwa kwa malengo ya utafiti, mipaka ya utafiti na nadharia za utafiti. Tulitumia hojaji kwa wanafunzi na walimu kutathmini mielekeo, kiwango cha uchanganuzi na ufasiri, pamoja na mbinu na hali nzima ya ufunzaji na ujifunzaji wa mashairi na ushairi shuleni. Tathmini hii iliegemezwa kwa vigezo vya ufasiri mwafaka wa Ki-Hemenitiki ambavyo ni ukubalifu, uwiano, ufaafu na mshikamano. Pia, tulitumia kazi mradi kwa wanafunzi hao kwa makusudi mawili: Tathmini ya umilisi kimsingi wa ushairi miongoni mwao na kutathmini uwezo wao wa ufasiri mashairi. Data iliyoibuliwa ilichanganuliwa kwa kutumia mbinu ya taraklishi ya uchanganuzi wa tarakimu sayansi za jamii. Matokeo yalidhihirishwa kwa viwango vya kiasilimia na kuwasilishwa kwa maelezo na ufafanuzi kwa takwimu majedwali na michoro duara. Utafiti umebaini kuwa ukengeushi wa Ki- Hemenitiki na kitamaduni ndio sababu kuu ya ufasiri na uhakiki mbaya wa ushairi miongoni mwa wanafunzi wa Sekondari Kenya. Utafiti umeweka bayana changamoto nyingi zinazokumba somo la ushairi ikiwa ni pamoja na mielekeo hasi miongoni mwa 50% ya wanafunzi hao, uhuru wa kupindukia wa kukabili somo la ushairi kwa walimu, matatizo ya lugha ya Kilahaja na Kikae, utahini wa kuyumbayumba, ukosefu wa mwongozo wa kufundishia kwa walimu, ukosefu wa vitabu teule na cha kiada cha ushairi na kwa jumla, ukosefu wa umilisi wa ushairi kwa wanafunzi miongoni mwa mengine. Utafiti huu umetoa mchango mufti katika taaluma ya ushairi wa Kiswahili hususan kuelewa jinsi ukengeushi wa Ki-Hemenitiki na kitamaduni unavyochangia ugumu wa ufasiri na uelewekaji wa ushairi. Hili limechangia katika kusuluhisha suala la ugumu wa ushairi miongoni mwa wanafunzi wa sekondari kwa kupendekeza jinsi viwango vya ukengeushi katika ufasiri vinavyoweza kuzibwa.

Item Type: Thesis (Masters)
Subjects: P Language and Literature > P Philology. Linguistics
Divisions: Africana
Depositing User: Geoffrey Obatsa
Date Deposited: 02 Nov 2017 08:52
Last Modified: 02 Nov 2017 08:52
URI: http://thesisbank.jhia.ac.ke/id/eprint/2601

Actions (login required)

View Item View Item